Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.

Serikali imeweka kipaumbele kikubwa katika  ujenzi wa miundombinu ya Umma  kwani ni muhimu kuwa na miundombinu mizuri na bora ili kutoa huduma bora na kurahisisha ufanyaji kazi hivyo kuharakisha maendeleo ya nchi katika nyanja zote muhimu zikiwemo za biashara, utalii na mawasiliano.

Matumizi makubwa ya fedha za Serikali yanatumika katika ujenzi wa miundombinu ya Umma ambapo matumizi hayo yanahusisha karibu asilimia 53 ya Bajeti nzima ya nchi.

Miradi ya ujenzi wa miundombinu ya Umma inayoelezewa hapa ni ile ambayo inajengwa kwa fedha za Serikali kwa ajili ya matumizi ya wananchi wote ikiwemo ya barabara, hospitali na vituo vya afya,shule na vyuo,nyumba za kuishi pamoja na ofisi mbalimbali. 

Ingawa Serikali inajitahidi kuhakikisha nchi inakuwa na miundombinu bora itakayochochea maendeleo, lakini jitihada hizo zimekuwa zikikwamishwa na changamoto mbalimbali zinazojitokeza pindi mradi husika unavyoanza kwani wahusika hawatumii fedha kama zilivyopangwa na badala yake wanafanya kwa makadirio ya chini na kufanya ujenzi kutokuwa imara.

Hali hiyo inasababisha Serikali kupata hasara kwa kupoteza fedha nyingi na kuambulia kubaki na majengo yasiyo na viwango ambayo mwisho wake hushindwa kutumika na kuilazimu Serikali kuanza upya ujenzi husika. 

Kwa kuwa Serikali hii ni sikivu na imejipanga kuhakikisha nchi inafika katika uchumi wa kati basi mambo hayo hayana nafasi na hayawezi kutokea tena katika nchi hii watu kuachiwa huru kutumia vibaya fedha za Umma zinazotolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu. 

Kwa kuhakikisha hilo,Serikali kupitia Baraza la Ujenzi la Taifa (NCC) chini ya Mkakati wa Kukuza Uwazi na Uwajibikaji katika Sekta ya Ujenzi Tanzania (CoST-Tanzania) imejipanga kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika sekta hiyo ili kuondokana na rushwa pamoja na ubadhilifu wowote wa fedha za Umma zinazotolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu hiyo.

Mkakati huo unalengo la kupambana na rushwa, usimamizi mbaya katika ujenzi pamoja na changamoto zingine zinazopelekea ubadhilifu wa fedha zinazotengwa kwa ajili ya miundombinu ya Umma kwa kukusanya taarifa za miradi hiyo ya ujenzi ili  kuhakikisha kama thamani ya miundombinu iliyojengwa inalingana na thamani ya fedha iliyotolewa kwa ajili ya ujenzi husika. 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano,(Ujenzi), Mha. Joseph Nyamuhanga alikaririwa akisema kuwa “Sekta ya Ujenzi ni sekta moja wapo inayoonekana kukithiri kwa rushwa duniani kwa sababu takribani asilimia 10 hadi 30 ya Bajeti yake inapotea kwa njia ya rushwa na usimamizi mbaya hivyo ili kuondoa dhima hii ni lazima kukusanya na kutoa taarifa kwa wananchi juu ya ujenzi wa miundombinu hiyo”.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...